MADAKTARI WALIJIFUNZA KUTOKANA NA HALI YANGU YA KUKARIBIA KIFO
“Siku iliyofuata kiwango changu cha hemoglobini kilikuwa kimeshuka hadi 2.9. Nilipoamka na kupata familia yangu yote kando ya kitanda changu, nilijiuliza ni nini kilikuwa kimetokea. Singeweza kuzungumza kwa sababu ya mashine ya kusaidia kupumua. Nilihisi hisia nyingi mno kwa huzuni, lakini singeweza hata kulia. Kila mtu aliniambia kwamba ilikuwa lazima nihifadhi nguvu zangu ili niweze kuokoka..”
BWANA YESU ASIFIWE SANA.,
Tulipata
kujua kwamba tulikuwa tukitazamia mtoto wetu wa nne. Mtoto wetu mdogo
Zaidi Mikael, alikuwa na umri wa miaka tisa, na mabinti wetu pacha,
Maria na Sara, walikuwa na miaka 13. Ingawa mtoto mwingine hakuwa
amepangiwa, baada ya muda mfupi tulikuja kuzoea wazo la kuwa na mtoto
mwingine.
Jioni moja katika mwezi wa tatu wa mimba, nilihisi maumivu ya ghafula
katika pafu langu. Siku iliyofuata singeweza kutembea hata kidogo.
Daktari
alisema kwamba nilikuwa na mchochota wa pafu, kisha akanipa
Peninsilini. Nilianza kuhisi vema baada ya siku kadhaa, lakini nilikuwa
mnyonge sana. Kisha ghafula nikapata maumivu katika pafu langu jingine,
na taratibu ileile ikarudiwa.
Siku zilizofuata, singeweza kulala kwa sababu ya ugumu wa kupumua. Zaidi
ya juma moja hivi baada ya shambulio la kwanza la maumivu, mmoja wa
miguu yangu ukawa rangi ya buluu na ukafura. Wakati huu nililazwa
hospitalini. Daktari alinijulisha kwamba maumivu katika mapafu yangu
hayakusababishwa na mchochota wa pafu bali migando ya damu. Yeye pia
alisema kwamba nilikuwa na mgando wa damu katika kinena changu. Nilipata
kujua kwamba migando ya damu ni moja ya visababishi vya kifo vya
kawaida miongoni mwa wanawake wajawazito. Siku chache baadaye,
nilihamishwa hadi Hospitali hiyo na kupelekwa hospitali nyingine, ambayo
ina kliniki ya kipekee ya ujauzito kwa ajili ya mimba zinazotatanisha.
Madaktari waliamua kunipa matibabu ya kuifanya damu kuwa nyepesi na
kutoganda upesi. Walinihakikishia kwamba hatari ya kutokwa damu kwa
sababu ya dawa ya kufanya damu kutoganda upesi ilikuwa ndogo
ikilinganishwa na hatari ya kupatwa na mgando mwingine mapafuni. Baada
ya majuma kadhaa, nilihisi nafuu vya kutosha kurudi nyumbani. Nilihisi
furaha yenye uchangamfu kwa kuwa hai pamoja na mtoto mdogo sana
aliyekuwa akikua ndani yangu.
SAA YA KUJIFUNGUA
Wakati wa kijifungua kulipokaribia, Iliamuliwa kwamba kuzaa kuchochewe,
lakini kabla ya hatua kuchukuliwa kuanza hiyo taratibu, nilihisi maumivu
makali mno katika sehemu ya chini ya fumbatio langu. Kwa hiyo
nikakimbizwa hospitali. Hata hivyo, madaktari hawakuweza kupata kasoro
yoyote.
Jioni iliyofuata fumbatio langu lilivimba sana, na maumivu hayakuwa
yamepungua. Katikati mwa usiku, daktari alinichunguza na kupata kwamba
nilikuwa katika uchungu wa kuzaa. Asubuhi iliyofuata fumbatio langu
lilivimba hata zaidi, na maumivu yalikuwa yasiyovumilika. Daktari
alionekana akiwa na wasiwasi kisha akauliza ni lini mara ya mwisho
nilipotambua kusogea-sogea kwa mtoto. Nilitambua ghafula kwamba ni muda
mrefu sana ulikuwa umepita.
Nilikimbizwa mara hiyo hadi kwenye chumba cha leba. Kwa mbali ningeweza
kusikia wafanyakazi wakizungumza. “Anakataa kutiwa damu mishipani,” mtu
fulani akasema. Kisha muuguzi mmoja akainama juu yangu na kusema kwa
sauti kubwa: “Unajua mtoto wako amekufa, sivyo?” Nilihisi kana kwamba
mtu alikuwa amechoma moyo wangu kwa upanga.—Mithali 12:18.
Mara daktari wangu akatokezea na kuniambia kwamba hali yangu ilikuwa
mbaya mno. Yeye aliuliza ikiwa bado nilitaka kushikamana na uamuzi wangu
wa kutokubali utiaji-damu mishipani. Nilitaarifu kwa uthabiti kwamba
nilishikamana na uamuzi wangu, lakini sikumbuki mengi baada ya hapo.
Hata hivyo, nilikuwa nimeweka wazi kabisa kwa daktari wangu kwamba
Wakristo wanaamriwa wajiepushe na damu na kwamba nilitaka kuwa mtiifu
kwa sheria ya Mungu.—Matendo 15:28, 29; 21:25.
Wakati
huohuo walimwita daktari mwingine, daktari-mpasuaji stadi. Yeye alifika
haraka na kufanya upasuaji mara hiyo. Walipofungua fumbatio langu,
waligundua kwamba nilikuwa nimepoteza lita tatu za damu kupitia kuvuja
damu kwa ndani. Lakini Dakt. alistahi uamuzi wangu kuhusu utiaji-damu
mishipani.
Baadaye, daktari mwingine alisema kwamba lilikuwa jambo la madakika tu
kabla ya mimi kufa. “Sijui kama angali hai saa hizi,” yeye akadai.
Baadaye ilijulikana kwamba hao madaktari hawakuweza kupata chanzo cha
mvujo wa damu, kwa hiyo wakaweka kipande cha kitambaa ili kufinya ndani
ya fumbatio langu. Madaktari na wauguzi hawakutoa tumaini lolote lile la
kuokoka kwangu.
Watoto wangu walipofika hospitalini na kujua kuhusu hali yangu, mmoja
wao alisema kwamba lipo tumaini karibuni na kwamba baada ya hapo
wataniona tena katika ufufuo. Jinsi ufufuo ulivyo mpango mzuri ajabu na
wa haki!—Yohana 5:28, 29; 11:17-44; Matendo 24:15; Ufunuo 21:3, 4.
UHAI WANGU HATARINI.
Hemoglobini yangu ilikuwa imeshuka hadi gramu nne kwa desilita, lakini
kuvuja damu kulionekana kulikuwa kumekoma. Mapema nilikuwa nimeweka
nakala ya gazeti la Amkeni! (Kiingereza) la Novemba 22, mwaka huo.
Katika mahali pa kuwekea rekodi za mgonjwa. Daktari alilipata na kuona
kichwa, “Kuzuia na Kudhibiti Kuvuja kwa Damu Bila Utiaji-Damu
Mishipani.” Yeye alilipitiapitia kwa hamu ili kuona ikiwa kulikuwa na
jambo ambalo angetumia ili kunisaidia kuokoka. Macho yake yaliangukia
neno “erythropoietin,” ambayo ni aina ya utibabu unaochochea mwili
kutokeza chembe nyekundu za damu. Sasa yeye aliutumia. Lakini utibabu
huo huchukua wakati kuwa na matokeo. Kwa hiyo swali lilikuwa, Je,
utibabu wa erythropoietin ungefanya kazi kwa wakati?
Siku iliyofuata kiwango changu cha hemoglobini kilikuwa kimeshuka hadi
2.9.
Nilipoamka na kupata familia yangu yote
kando ya kitanda changu, nilijiuliza ni nini kilikuwa kimetokea.
Singeweza kuzungumza kwa sababu ya mashine ya kusaidia kupumua. Nilihisi
hisia nyingi mno kwa huzuni, lakini singeweza hata kulia. Kila mtu
aliniambia kwamba ilikuwa lazima nihifadhi nguvu zangu ili niweze
kuokoka.
Siku iliyofuata nilipata homa kwa sababu ya kuvimba kulikosababishwa na
kile kitambaa cha kufinya kilichoachwa katika fumbatio langu.
Hemoglobini yangu ilikuwa imeshuka hadi 2.7. Ingawa ni hatari mno kumtia
mtu unusukaputi katika hali hiyo, Daktari alielezea kwamba licha ya
hiyo hatari, walilazimika kufanya upasuaji tena ili kuondoa kitambaa cha
kufinya.
Kabla ya upasuaji watoto waliruhusiwa kuja ndani kuniona. Kila mtu
alifikiri ilikuwa kwaheri ya kuonana. Washiriki kadhaa wa wafanyakazi wa
kitiba walikuwa wakilia. Hawakuamini ningeokoka. Watoto wetu walikuwa
jasiri sana, na hili lilinifanya niwe mtulivu na mwenye uhakika. Kwa
kuwa nusukaputi niliyopewa ilikuwa chache, nyakati fulani ningeweza
kusikia kile wafanyakazi walichokuwa wakisemezana.
Wengine
waliongea kunihusu kana kwamba nilikuwa mfu tayari. Baadaye,
niliposimulia kile nilichokuwa nimesikia wakati wa upasuaji, muuguzi
mmoja aliomba msamaha. Lakini alisema alikuwa na uhakika kwamba nilikuwa
nife na bado hakuelewa jinsi nilivyookoka.
Siku iliyofuata nilihisi nafuu kidogo. Hemoglobini yangu ilikuwa 2.9, na
hematokriti ilikuwa 9. Ndugu na dada zangu wa Kikristo walinitembelea,
wakiletea familia yangu chakula na kahawa. Tulishukuru kwa upendo na
shauku yao. Kufikia jioni hali yangu ilikuwa mbaya bado lakini thabiti,
na nilihamishwa kwa wodi nyingine.
Washiriki wengi wa wafanyakazi wa kitiba walikuwa wadadisi kunihusu, na
wengi wao walikuwa wenye fadhili. Muuguzi mmoja alisema hivi:
“Ni
lazima Mungu wako alikuokoa.” Daktari kutoka wadi nyingine alikuja na
kusema hivi: “Nataka tu kuona jinsi mtu mwenye hemoglobini ya chini
hivyo anavyofanana. Siwezi kufahamu jinsi unavyoweza kuwa macho namna
hiyo.”
Siku iliyofuata, ingawa ilikuwa siku yake ya likizo, daktari wangu
alikuja kuniona. Yeye aliniambia kwamba alihisi unyenyekevu kwa sababu
ya kilichotukia. Ikiwa ningepata nafuu kabisa, yeye akasema,
wangeanzisha utafiti mpya katika vibadala ya tiba ya utiaji-damu
mishipani katika kutibu wagonjwa.
Kupona kwangu kulikuwa kwenye kutazamisha. Majuma mawili na nusu baada
ya kujifungua kwangu kwa kimsiba, kiwango changu cha hemoglobini
kilikuwa kimeongezeka hadi kidogo zaidi ya 8. Kwa hiyo niliruhusiwa
kutoka hospitalini. Siku tatu baadaye tulikuwa na kusanyiko letu na
wapendwa nyumbani, nami nilikuwako pale.
Jinsi
ilivyotia moyo kuona tena ndugu na dada zetu wa Kiroho ambao walikuwa
wenye kutegemeza wakati wa shida yetu!—Mithali 17:17.
TUNAMTUKUZA YESU SANA..Amen.
####################
JE, UNA USHUHUDA AMBAO UNGEPENDA TUUCHAPISHE??
Fanya hivyo ili maelfu wajue mambo ambayo MUNGU alikutendea na kupitia ushuhuda wako maelfu ya wasomaji watayashuhudia matendo ya Mungu uliyenaye.
Aisee Mungu Ni mwaminifu
ReplyDeleteAmina,Mungu Anatenda mambo makuu
ReplyDelete